Monday, September 26, 2011

SIMBA JUU KWA JUU YATAFUNA MIWA YA MTIBWA, KAGERA SUGAR YATOA DOZI KWA POLISI

















Uhuru Selemani akichanja mbuga

MSHAMBULIAJI Emmanuel Okwi alitia kambani bao pekee na kuipaisha Simba kileleni mwa Ligi Kuu katika mechi dhidi ya Mtibwa Sugar, pia Kagera Sugar imepata ushindi wake wa kwanza msimu huu baada ya kuilaza Polisi Dodoma mabao 2-0.

Simba ambao walishuka kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam wakiwa na kumbukumbu ya kulazimishwa sare mara mbili Kanda ya Ziwa iliwachukua dakika 35 kabla ya mashabiki wake kufurahi baada ya Okwi kupokea vizuri pasi ya Uhuru Seleman na kufunga bao hilo kwa shuti kali ambalo limeiwezesha Simba kufikisha pointi 18.

Pamoja na ushindi huo wa bao 1-0 ilioupata Simba, beki wa timu hiyo Victor Costa alikosa mkwaju wa penalti katika dakika ya 90 baada ya mkwaju wake kupanguliwa na kipa wa Mtibwa Sugar, Deogratius Munishi"Dida"

Mabingwa wa mwaka 2000, Mtibwa Sugar walianza mechi kwa kishindo kupitia Masoud Ally aliyepokea pasi ya Thomas Maurice na kupiga shuti kali la umbali wa mita 25, lililopanguliwa na kipa wa Simba, Juma Kaseja.

Simba walijibu mapigo katika dakika ya nane kupitia kwa Uhuru Seleman aliyetokea winga ya kushoto na kutoa pasi kwa Emmanuel Okwi aliyepiga shuti lililopaa juu.

Mtibwa waliendelea kupeleka mashambulizi katika lango la Simba, ambapo walipata faulo ambayo ilipigwa na Masou Ally katika dakika ya11 na mpira uligonga mwamba na mabeki wa Simba waliokoa mpira huo na kuwa kona.

Pia Simba na wenyewe waliendelea kulishambulia lango la Mtibwa ila katika dakika ya 13 Okwi alishindwa kutumia vizuri pasi ya Jerry Santo kufunga bao.

Mechi hiyo pia ilisimama kwa dakika kadhaa baada ya kiungo Zuberi Katwila wa Mtibwa kugongana na Victor Costa wakati wakiwania mpira wa juu na wote wawili walitolewa nje kwa ajili matatibu, lakini walitibiwa na kurudi kuendelea na mchezo.

Lakini hali ya Katwila ilionekana siyo nzuri kwani alikuwa akichechea na aliomba kutoka hivyo kocha wa Mtibwa Sugar, Tom Olaba alilazimika kumtoa Katwila katika dakika ya 22 na kumwingiza Awadhi Juma.

Chipukizi Shomari Kapombe wa Simba katika mechi hiyo alikosa bao dakika ya 28 baada ya shuti lake kumgonga beki wa Mtibwa na kuwa kona ambayo haikuleta madhara.

Kapombe pia alitengeneza pasi nzuri kwa Uhuru aliyemchungulia Okwi ambaye aliutumia vizuri udhaifu wa nahodha wa zamani wa Taifa Stars, Salum Sued aliyeoneka kushindwa kwenda na kasi ya mchezo kufunga bao la Simba katika dakika ya 35.

Mtibwa walirudi kwa kasi katika kipindi cha pili, ambapo katika dakika ya 47, nusura wasawazishe baada ya krosi ya kiungo Shabaan Nditi kutua kichwani mwa Maurice ambaye alipiga nje.
Katika dakika ya 90, Simba walipata penalti baada ya Haruna Moshi kuangushwa kwenye eneo la hatari na mwamuzi David Paulo kutoka Mtwara kuamuru adhabu hiyo.

Beki wa Simba, Costa alishindwa kutoa zawadi ya bao kwa mtoto wake watatu wa kiume aliyezaliwa juzi baada ya mkwaju wake wa penalti kupanguliwa na kipa wa Mtibwa Sugar, Munishi katika dakika ya 90.

Kocha Olaba wa Mtibwa katika mechi hiyo alimtoa Ally Mohamed na kumwingiza Hussen Javu wakati, Moses Basena wa Simba aliwatoa Uhuru Selemani ,Amri Kiemba na Gervais Kago na kuwaingiza Ulimboka Mwakingwe, Shija Mkina na Haruna Moshi.

Akizungumza baada ya mechi hiyo kumalizika kocha wa Mtibwa, Olaba alisema wachezaji wake hawakucheza vizuri katika kipindi cha kwanza, lakini walibadilika dakika 45 za mwisho.

"Viungo walikosa maelewano katika kipindi cha kwanza, lakini tuliporudi mapumziko walibadilika na kufanya vile tulivyotaka."

KAGERA: Wenyeji Kagera Sugar baada ya kupokea kipigo cha mabao 2-0 kutoka kwa Oljoro katikati ya wiki walibadilika jana na kuichakaza Polisi Dodoma mabao 2-0 kwenye Uwanja wa Kaitaba mjini Bukoba.

Washambuliaji Hussein Sued na Said Dilunga walitia kambani mabao mawili katika kipindi cha kwanza na kurudisha imani ya wanakagera kwa timu yao ambayo imepata ushindi huo kwa mara ya kwanza.

Sued alifunga bao la kwanza kwa mkwaju wa penalti dakika ya kumi baada ya Dilunga kuangushwa kwenye eneo la hatari na beki wa Polisi, Frank Sindato na mwamuzi Amon Paul kutoka mkoani Mara kuamuru penalti.

Wakati maafande hao waliokuwa chini ya kocha msaidizi wakijiuliza nini kinatokea Sued alipitisha krosi nzuri iliyomkuta Dilunga aliyesukuma mpira wavuni na kuwainua mashabiki wa Kagera Sugar waliojitokeza kwenye uwanja huo.

Kagera Sugar iliwapumzisha Malegesi Mwanga, Sunday Frank, Sued na kumwingiza Khamis Ally na Temmy Felix, Ibrahim Mamba, Katika mechi hiyo Polisi iliwapumzisha Raygan Mbuta na Delta Nyamancheja na nafasi zao kuchukuliwa na Ibrahim Masawe na Haruna Hassan.
Pia katika mchezo huo wenyeji walioneka kucheza kwa kujiamini na kuelewana tofauti na ilivyokuwa walipocheza dhidi ya Oljoro.

Ligi hiyo inaendelea leo kwa Azam wanaoshika nafasi ya pili kuwavaa Ruvu Shooting kwenye Uwanja wa Mabatini Mlandizi, wakati Chamazi, JKT Ruvu watakuwa na kibarua kizito mbele ya Villa Squad huku jijini Mwanza Toto African watakuwa wenyeji wa Oljoro JKT kwenye Uwanja wa CCM Kirumba.

Katika hatua nyingine Shirikisho la soka Tanzania limetangaza viingilio vya mchezo kati ya Yanga na Coastal Union kuwa ni sh 3,000 kwa viti vya bluu na kijani, sh 5,000 kwa viti vya rangi ya chungwa VIP C ni sh 7,000, VIP B ni sh 10,000 na VIP A itakuwa sh. 15,000.

VIDEO ZA MATUKIO NA MAGOLI KATIKA MECHI ZA MWISHO WA WIKI LIGI MBALIMBALI DUNIANI

                                                       LIGI KUU UINGEREZA 

                                               Newcastle United 3-1 Blackburn Rovers


Stoke City 1-1 Man United



Wigan Athletic 1-2 Tottenham Hotspurs


Manchester City 2-0 Everton


LIGI KUU UJERUMANI

Bayern Munich 3-0 Bayer Leverkusen


LIGI KUU ITALIA

AC Milan 1-0 Cesena


Bologna 1-3 Inter Milan


LIGI KUU UHOLANZI

PSV Eindhoven 7-1 Roda JC


LIGI KUU UHISPANIA

Real Madrid 6-2 Rayo Vallecano


Barcelona 5-0 Atletico Madrid











Friday, September 23, 2011

Claudio Ranieri akabidhiwa mikoba ya Gian Piero Gasperini Inter Milan

Kocha wa zamani wa Chelsea Claudio Ranieri ametangazwa kuwa kocha mpya wa Inter Milan kwa mkataba unaokwenda hadi mwaka 2013.
Ranieri
Kocha mpya wa Inter

Tangazo hilo limefuatia kufukuzwa kazi kwa Gian Piero Gasperini siku ya Jumatano asubuhi.
Gasperini alisimamishwa kazi baada ya kufungwa mechi nne na kutoka sare mchezo mmoja katika mechi tano ambazo alikuwa akiongoza kikosi hicho.
Gasperini alikuwa amechukua nafasi ya Leonardo mwezi Juni.
Gasperini
Gasperini

Hii itakuwa kazi ya kwanza kwa Ranieri tangu alipoondoka Roma mwezi Februari kutokana na kupoteza mechi nne mfululizo.
"Claudio Ranieri sasa ni kocha rasmi wa Inter," imesema taarifa ya klabu hiyo siku ya Alhamisi.
Chini ya Gasperini, Inter ilifungwa 3-1 dhidi ya timu iliyopanda daraja msimu huu Novara, siku ya Jumanne, na kupoteza michezo dhidi ya Palermo kwenye ligi kuu, Trabzonspor katika Klabu Bingwa Ulaya, na kwa mahasimu wao AC Milan kwenye mchezo wa kombe la Italia.
Mchezo pekee katika uogozi wa Gasperini uliomalizika bila kufungwa ni sare ya 0-0 dhidi ya Roma wiki iliyopita.
Hata hivyo Ranieri ambaye aliwahi pia kuwa kocha wa Juventus amekuwa akisuasua kushida vikombe. Kombe la mwisho aliloshinda lilikuwa la Italian Cup mwaka 1996 akiwa na Fiorentina, na pia kombe la Hispania akiwa na Valencia miaka mitatu iliyofuatia.

Bob Bradley amrithi Shehata timu ya taifa ya Misri

Kocha wa zamani wa timu ya taifa ya Marekani, Bob Bradley, Alhamisi ametangazwa kuwa sasa ni kocha mpya wa timu ya taifa ya Firauni ya Misri.
Mkataba wa Bradley utaendelea hadi fainali za Kombe la Dunia nchini Brazil, kufanyika mwaka 2014.
Bob Bradley
Anachukua ukocha kutoka kwa Hassan Shehata aliyejiuzulu baada ya mfululizo wa matokeo ya kutoridhisha
Atakuwa akipokea mshahara wa dola za Marekani 40,000 kwa mwezi.
Kulikuwa na fununu kwamba Bradley alitazamiwa kuiongoza timu ya Misri ya Firauni, na aliweza kupata mkataba huo baada ya mashauri na chama cha soka cha Misri mjini Cairo.
Anatazamiwa kuitisha mkutano na waandishi wa habari siku ya Jumamosi, ili kuelezea mipango yake, katika kuinyanyua timu hiyo ambayo imekuwa ikifanya vibaya hivi majuzi.
Misri imetwaa ushindi katika awamu tatu za fainali ya mashindano ya Kombe la Mataifa ya Afrika, lakini wakati huu imeshindwa kufuzu kushirikishwa katika fainali zijazo kufanyika katika mataifa ya Equatorial Guinea na Gabon mwaka 2012.
"Wachezaji wa Misri ni wazuri mno," alielezea mara tu baada ya kufika Cairo.
"Nchini Marekani tulijitahidi kuwaimarisha wachezaji katika nyanja zote; kiufundi, kimaarifa, miili yao pia, na nadhani ni muhimu kufanya hivyo."
Hisia za mashabiki na vyombo vya habari hazijajitokeza waziwazi kufuatia Bradley kutangazwa kama kocha mpya nchini Misri.
Bradley awali alitazamiwa kuwasili Misri siku ya Jumanne, lakini akacheleweshwa kutokana na matatizo katika kupata ndege.
Chama cha soka cha Misri (EFA), kilikuwa kimefikiria pia kumpa kazi hiyo kocha wa zamani wa Ghana, Milovan Rajevac, lakini hatimaye kikaamua kumwajiri Bradley.
Bradley anachukua wadhifa ulioachwa wazi na Hassan Shehata, ambaye aliamua kujiuzulu kutokana na mfululizo wa matokeo mabaya katika mechi za awali za kufuzu kushirikishwa katika fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika 2012.
Timu ya Firauni, licha ya kwamba hawana tena nafasi ya kufuzu kwa mashindano hayo, watakuwa ni wenyeji wa timu ya Niger, katika mechi yao ya mwisho ya kufuzu mwezi Oktoba.

Thursday, September 22, 2011

Barcelona Valencia nguvu sawa 2-2

Timu ya Valencia ilifanikiwa kutoka sare na Barcelona katika mechi ya Ligi ya Spain inayoendelea nchini humo. Magoli ya Valencia yalifungwa na Abidal dk 12 aikijifunga na Hernandez dk 23 wakati ya Barcelona yalifungwa na Pedro dk 14 na la pili Fabregas dk 77.

Yanga,Azam mbele kwa mbele Simba yatoa sare na Toto Africans















Asamoah akijaribu kuwatoka walinzi wa Villa

Timu ya soka ya Yanga wamewanyuka Villa Squad wakiwa pungufu kwa "bakora" 3-2 kwenye Uwanja wa Chamazi huku vinara wa ligi Simba wakilazimisha sare ya 3-3 na Toto African jijini Mwanza.Wakati Yanga wakipata ushindi wao wa pili na kufikisha pointi tisa, matajiri wa Chamazi, Azam wenyewe wamesogea hadi nafasi ya pili kwenye msimamo kwa kufikisha pointi 14 na kuisogelea Simba inayoongoza kwa pointi 15 baada ya kupata sare ya tatu katika mechi saba.

Macho ya wengi yalikuwa Uwanja wa Chamazi, ambapo Yanga ilipokuwa na kibarua kizito mbele Villa Squad waliokuwa wa kwanza kupata bao kupitia Nsa Job, lakini mabingwa hao walisawazisha kupitia Haruna Niyonzima na Kenneth Asamoah na Hamis Kiiza waliongeza mabao mengine kabla ya Kigi Luseke kuifungia Villa bao la pili na kufanya matokeo kuwa 3-2.

Azam wenyewe wakiwa ugenini itabidi wamshukuru John Boko kwa kuwafungia bao pekee katika mechi dhidi ya Coastal Union akimalizia penalti yake iliyotemwa na kipa.

Katika mechi ya Yanga dhidi ya Villa, nyota wa kimataifa wa Yanga walilipa fadhila kwa kufunga mabao na kumpunguzia presha kocha wao Sam Timbe aliyepewa mechi tatu za kuhakikisha anapata ushindi.

Mshambuliaji Mwape alikosa bao katika dakika ya tano kwa kushindwa kuunganisha krosi ya Ally Shamte iliyotoka sentimita chache kutoka goli la Villa Squad.

Kenneth Asamoah naye alikosa bao baada ya kuunganisha kwa kichwa krosi ya Oscar Joshua na kutoka nje, wakati nyota hao wa Yanga wakikosa Nsa Job alitumia vizuri mwanya wa kipa Yaw Berko kutoka kwenye mstali na kuinua mpira juu na kujaa wavuni katika dakika ya 11.

Dakika nne baadaye Niyonzima aliisawazishia Yanga bao kwa mpira wa adhabu ambao aliupiga na kwenda moja kwa moja wavuni na kufanya matokeo kuwa 1-1.Kocha wa Villa Squad, Said Chamosi alimtoa Haruna Shamte katika dakika ya 24 na kumwingiza Evalist Maganga.

Kocha wa Yanga, Sam Timbe alimwaanzisha kwa mara ya kwanza Idrisa Rashid akicheza na Asamoah katika safu ya ushambuliaji ya timu hiyo.Matunda ya Rashid yalionekana baada ya mchezaji huyo kupitisha krosi nzuri kwa Asamoah aliyefunga bao lake la kwanza katika Ligi Kuu ya Tanzania na kuifanya Yanga kuongoza mabao 2-1 katika dakika ya 27.

Mshambuliaji huyo wa kimataifa wa Ghana alipoteza nafasi kadhaa za kufunga katika kipindi hicho cha kwanza, huku kocha Timbe akimweka jukwaani Jerryson Tegete aliyefunguliwa jana na uongozi wa Yanga.

Villa Squad walipata pigo dakika ya 57 baada ya mwamuzi Ibrahim Kidiwa kumuonyesha kadi nyekundu, Stamili Mbonde kwa kudanganya baada ya kujiangusha na kupewa kadi ya njano ya pili.

Kocha Timbe aliwatoa Asamoah, Mwape na Shamte na kuwaingiza Rashid Gumbo, Hamis Kiiza na Juma Seif, huku Villa wakimpumzisha Lameck Dayton na kumwingiza Kigi Luseke.

Mabadiliko hayo yalikuwa na faida kwa Yanga, ambapo dakika ya 63 Kiiza alifunga bao la tatu kwa mabingwa hao akiunganisha pasi ya Rashid ambaye ameonyesha soka ya kiwango cha juu katika mechi hiyo.

Villa Squad walipata bao la pili kwa shuti la mita 20 lililopigwa na Luseke, baada ya mabeki wa Yanga kuzubaa kuokoa mpira katika dakika ya 72 na kumwacha kipa Berko asijue la kufanya.

MWANZA; Kanda ya ziwa kumeonekana kuwa kugumu kwa vinara wa ligi Simba kufuatia kulazimisha sare nyingine ya mabao 3-3 baada ya ile ya 1-1 waliyopata mwishoni mwa wiki dhidi ya Kagera Sugar.

Katika mechi hiyo mshambuliaji Felix Sunzu alifunga mabao mwili peke yake, lakini hayakutosha kuipa pointi tatu Simba mbele ya Toto African kwenye uwanja CCM Kirumba.

Sunzu alifungia Simba bao kwanza katika dakika ya 7, kabla ya wenyeji Toto Afrika kuamka na kusawazisha na kupata bao la kuongoza mabao yote mawili yakifungwa na Enyema Darlington.

Mzambia Sunzu alipachika bao la pili Simba na kusawazisha akimalizia kazi nzuri ya Emmanuel Okwi, lakini Toto walifunga bao la tatu kupitia Soud Mohamed kabla ya Patrick Mafisango kuwasawazisha vinara hao na kufanya timu hizo kugawana pointi.

Mchezo huo ulishuhudia matukio kadhaa katika dakika ya 15 mashabiki walivunja geti la uwanja na kuingia uwanjani, lakini polisi waliweza kuthibiti tukio hilo kabla ya mbwa wa polisi kumponyoka askari na kuingia uwanjani na kuanza kukimbiza wachezaji na alimfukuza zaidi Haruna Moshi na kusababisha mpira kusimama kwa dakika tano katika dakika ya 29.

Pia katika mechi hiyo Simba ilipata pigo baada ya nyota wao Sunzu kuumia na kupoteza fahamu katika dakika ya 42 na kukimbizwa hospitali kwa matibabu zaidi.

TANGA, Mshambuliaji John Boko ameendeleza makali yake ya kuzifumania nyavu baada ya kuifungia Azam bao la kuongoza katika dakika 32 kwa kupiga penati iliyopanguliwa na kipa wa Coastal Union, Omari Hamis na kurudi uwanjani ambako aliuwahi na kumaliza kwa kichwa na kufunga bao hilo.

Mwamuzi Ronald Swai wa Arusha alitoa penati kwa Azam baada ya Boko kuangushwa kwenye eneo la hatari na beki Soud Juma wa Coastal Union na kufanya matokeo kuwa 1-0 hadi mapumziko.

Jinamizi la kukosa penati liliendelea kuiandama Coastal Union baada ya mkwaju wa Mohamed Ibrahim kupanguliwa na kipa Mwidadi Ally wa Azam kufuatia mshambuliaji Ben Mwalala kuchezewa vibaya kwenye eneo la hatari na beki Waziri Salum wa Azam dakika ya 68.

Wakati huohuo, Ligi kuu ya Vodacom Tanzania bara inaendelea tena leo kwenye viwanja vitatu tofauti, ambapo kwenye Uwanja wa Chamazi jijini Dar es Salaam, JKT Ruvu watavaana na Moro United, huku kwenye uwanja wa Jamhuri Dodoma, wenyeji Polisi Dodoma watawakaribisha Mtibwa Sugar na Kagera Sugar watakuwa wenyeji wa JKT Oljoro.

Kwenye uwanja wa Chamazi, JKT Ruvu wanaoshika nafasi ya nne wakiwa na pointi kumi wanashuka kwa lengo moja tu la kusaka ushindi dhidi ya Moro United yenye machungu ya kuchapwa mabao 5-2 na Polisi Dodoma.

Kocha wa JKT Ruvu, Charles Kilinda alisema anaingia uwanjani akiwa na kumbukumbu ya kutoka sare na Toto katika mchezo uliopita hivyo ushindi wa leo ni lazima baada ya majeruhi wake kuwa katika hali nzuri kiafya na kuahidi kuwatumia leo.

Tuesday, September 20, 2011

Mourinho aigawa zawadi ya kocha bora wa Dunia kwenye mfuko wa Bobby Robson


Mourinho akimkabidhi zawadi hiyo

Bosi wa Real Madrid Jose Mourinho ametoa zawadi yake ya kujivunia ya kocha bora wa mwaka ili ipigwe mnada na fedha ziingizwe katika mfuko wa Sir Bobby Robson unaopambana na kansa.
Mourinho amefanya kazi na Bobby akiwa Sporting Lisbon,Porto na Barcelona na kujifunza kuwa meneja bora wa timu.
Mourinho atatoa tuzo hiyo ya kocha bora wa dunia aliyoipata akiwa na klabu ya Inter Milan 2010 na itapiogwa mnada katika mtandao mwezi ujao na yule atakae dau kubwa ndio atainyakua tuzo hiyo na fedha kuelekezwa kwenye mfuko wa Sir Bobby Robson.
Mnada huo utafanyika kuanzia tarehe 8-23 sambamba na mchezo wa hisani wa soka katika uwanja wa Burry St Edmunds,Suffolk.