Wednesday, August 10, 2011

LIGI YA UINGEREZA KUAHIRISHWA KUTOKANA YA MACHAFUKO NCHINI HUMO

Waandaaji wa Ligi Kuu ya soka ya England, wataamua siku ya Alhamisi iwapo michezo ya ufunguzi wa msimu mpya wa ligi iahirishwe au la baada ya ghasia kuendelea usiku wa kuamkia siku ya Jumanne.
Ghasia mjini Manchester
Ghasia mjini Manchester

Ghasia zimekuwa zikiendelea sehemu mbalimbali nchini Uingereza tangu siku ya Jumamosi, hali inayowafanya askari polisi wawe na kazi nyingi zaidi.
Taarifa ya pamoja iliyotolewa na Premier League imesema: "Tupo katika mazungumzo na vilabu vya London, polisi na mamlaka nyingine zinazohusika.
"Taarifa zaidi zitatolewa baada ya kutathmini hali ilivyo katika mkutano wa Alhamisi."
Kuna ratiba ya mechi tatu za Ligi Kuu ya England zitakazochezwa siku ya Jumamosi: Tottenham v Everton, Fulham v Aston Villa na QPR v Bolton.
Taarifa iliyotolewa siku ya Jumanne, imesema"hakuna sababu za kufikiria iwapo mechi nje ya London zitaathirika ", lakini hayo yalizungumzwa kabla ghasia hazijaenea hadi mji wa Manchester.
West Bromwich itaikaribisha Manchester United siku ya Jumamosi saa kumi jioni, kabla ya Manchester City kupambana na Swansea siku ya Jumatatu saa mbili usiku.
Ratiba za mechi kadha tayari zimeathirika kutokana na ghasia hizo. Mechi ya kirafiki ya kimataifa kati ya England na Uholanzi iliyokuwa ichezwe siku ya Jumatano imeahirishwa, Ghana na Nigeria pia mchezo wa kimataifa wa kirafiki nao ukaahirishwa uliokuwa ufanyike siku ya Jumanne.
Mechi ya kufuzu kwa Kombe la Carling kati ya Bristol Rovers na Watford pia ziliahirishwa kutokana na ushauri wa polisi, kufuatia kufutwa kwa mechi nyingine siku ya Jumanne za Charlton, West Ham, Crystal Palace na Bristol City.

No comments:

Post a Comment