Wednesday, November 9, 2011

Aspirini ni kinga ya saratani

Wataalamu wa tiba wameshauri kua watu ambao afya yao inakabiliwa na uwezekano wa kukumbwa na saratani ya kibofu, wapewe dozi ya aspirini.
Jarida linalochapisha habari za utafiti wa wataalamu ''The Lancet'' limearifu kua tembe mbili kwa kila siku zilipunguza saratani ya kibofu kwa asili mia 63% kati ya kundi la wagonjwa 861.
Wataalamu wengine wamesema kua utafiti huo umetoa mwangaza mpya kwamba aspirini inaweza kutumika katika kutibu saratani kwa ujumla.
Utafiti huu ulifanywa kwa kutumia wagonjwa 861 waliorithi maradhi haya ya saratani ya kibofu, ambayo huathiri mtu mmoja kati ya watu 1,000.
Kuna tatizo la kugundua wagonjwa kama hawa waliorithi magonjwa kama haya na tiba ya viini vya urathi huwa kazi kubwa, ikimaanisha kwamba kuna uwezekano kwao kukumbwa na maradhi kama saratani ya kibofu, kizazi na tumbo.
Uchunguzi wa wagonjwa wote wakati wa majaribio, wale waliokua katika kundi lililopewa miligramu 600 ya vidonge vya aspirini kwa kila siku, 19 kati yao walipatikana na uvimbe ikilinganishwa na uvimbe uliopatikana miongoni mwa wagonjwa ambao walikua wakitazamwa kwa karibu sana, ambao kiwango cha uvimbe kilipungua kwa asili mia 44.

Wataalamu hawa walipochunguza wagonjwa pekee waliotumia dawa hii kwa kipindi cha miaka miwili wakakuta kuna upungufu wa asili mia 63%.

Vilevile tiba hii ina athari juu ya saratani nyingine za uruthi, ambazo pia zilishuka kwa kadiri ya nusu kwa wagonjwa wanaochunguzwa kwa makini.
Profesa Sir John Burn, kutoka Chuo kikuu cha Newcastle alisema kua watu wazima 30,000 nchini Uingereza walirithi saratani ya kibofu.
Profesa Burn aliongezea kusema kua ikiwa watu hao watapewa matibabu basi tutapunguza saratani elfu kumi katika kipindi cha miaka 30 na kuonelea kua hilo linaweza kuepusha vifo takriban 1,000 kutokana na maradhi haya.
Hata hivyo, kuna athari zake pia.
"tukiweza kupunguza saratani 10,000 na kuzusha madonda ya tumbo 1,000 pamoja na kuondoa mishtuko ya moyo 100, kwa fikra za watu wengi ni bora kuliko kusubiri vifo, alisema Profesa Burns.
"watu wenye asili ya familia ambayo huathiriwa na magonjwa ya aina hii, hususan saratani ya kibofu ingefaa wajaribu dozi ndogo ya asipirini kama tabia."
Tangu hapo Aspirini ina sifa ya kupunguza maradhi ya mshituko wa moyo na kiharusi.
Utafiti mwingine katika kipindi cha miongo miwili iliyopita umeonyesha kua dawa aspirini hupunguza hatari ya saratani, ingawa utafiti huu wa sasa ndio wa kwanza kwa kutumia wagonjwa katika majaribio na kuhakiki aspirini katika kutibu saratani.
Moja ya maswali yaliyoulizwa kuhusu utafiti huu ni kama watu ambao hawana matatizo ya afya wala familia zenye historia ya ugonjwa huo wanaweza kutumia dawa hii.
Jibu likawa kua matumizi ya aspirini yanapunguza uwezekano wa saratani na maradhi ya moyo, kwa hiyo ni vizuri lakini kuna athari zake pia. Kwa Profesa Sir John, ni hoja nzuri hio kwa sababu yeye binafsi anaonelea kua athari za dawa hio ikilinganishwa na kiwango cha kuepuka saratani na maradhi ya moyo ni ndogo.
Hata hivyo anaonya kua atakayeamua kutumia aspirini kuepusha balaa la saratani, kiharusi au maradhi mengine ya moyo lazima achukue tahadhari. Matumizi ya dawa hio huongeza uwezekano wa madonda tumboni, kutokwa damu ndani ya tumbo ingawa wataepuka kiharusi kwa kutumia aspirini."

No comments:

Post a Comment