Friday, May 18, 2012

JEZI NAMBA 30 KUTOTUMIKA TENA SIMBA KATIKA KUMUENZI MAREHEMU PATRICK MUTESA MAFISANGO


Patrick Mutesa Mafisango akiwa na jezi namba 30

Habari za kuthibitika kutoka ndani ya klabu ya Simba ya Dar es salaam ambao ni mabingwa wa soka Tanzania bara 2012-2013 zinasema jezi namba 30 iliyokuwa ikitumiwa na kiungo mkabaji marehemu Patrick Mutes Mafisango imepigwa "STOP" kutumika au kuvaliwa na mchezaji mwingine katika hali ya kumuenzi mchezaji huyo wa kimataifa kutoka Rwanda.


Wachezaji wa Simba Uhuru Selemani na Yondani wakiwa katika majonzi hospitali ya muhimbili

Uhuru Suleiman ameshindwa kujizuia akimwaga chozi katika hospitali ya Taifa Muhimbili

Patrick Mutesa Mafisango alifariki siku ya alhamisi alfajiri saa 10:25 akitokea Muziki kuelekea nyumbani kwake keko. Ajali hiyo ilitokea maeneo ya Tazara jijini Dar es salaam kwa kile kilichosemekana marehemu alikuwa katika jitihada za kuokoa maisha ya muendesha pikipiki ndipo alipojaribu kumkwepa kwa kuwa gari ilikuwa katika mwendo kasi iliacha njia na kuingia mtaroni na kupinduka na kusababisha kifo cha mchezaji huyo papo hapo na wenzake aliokuwa nao kwenye gari kujeruhiwa.


Mashabiki wa Simba na wapenzi wa Mafisango wakiwa katika Hospitali ya Taifa Muhimbili

Hii ndiyo gari aliyopata nayo ajali Patrick Mutesa Mafisango

Kifo cha Mafisango kimeacha majonzi sio tu kwa Mashabiki na wachezaji wa Simba bali watanzania wote wapenda michezo na Wanyarwanda wote ambapo walikuwa wakimtegemea kwenda kujiunga na timu yao ya Taifa kupeperusha bendera ya Rwanda katika mashindano ya kutafuta nafasi ya kucheza kombe la dunia.


Boniface Pawasa mchezaji wa zamani wa Simba ameshindwa kabisa kujizuia akitokwa na machozi mbele yake ni Uhuru Suleiman

Wasanii wa kundi la Wanaume kushoto Chege na wenzake wakiwa msibani nyumbani kwa Mafisango

Haruna Moshi "Boban" akiwa katika lindi la majonzi akimlilia Mafisango

Kitu cha kusikitisha na kuhuzunisha zaidi ni kwamba Patrick Mutesa Mafisango baada ya kuitwa kujiunga na kikosi cha timu ya soka ya Taifa ya Rwanda na kocha Micho, aliomba asogezewe siku kwani alikuwa ndio ametoka kushiriki mashindano ya kombe la shirikisho akiwa na timu yake ya Simba ya Dar es salaam. Alipokubaliwa Patrick Mutesa Mafisango alikuwa amepanga kuondoka Tanzania leo 18/5/2012 kwenda kujiunga na timu yake ya Taifa ya Amavubi lakini kwa masikitiko siku hiyohiyo aliyoipanga kwenda Rwanda kujiunga na Timu yake sasa anakwenda akiwa hana uhai tena...inasikitisha sana!! MUNGU AILAZE ROHO YA PATRICK MUTESA MAFISANGO MAHALA PEMA PEPONO..AMIN!

No comments:

Post a Comment