Thursday, August 16, 2012

MGHANA WA SIMBA KUIKOSA LIGI KUU, YAWANIA JEMBE LINGINE KUTOKA MALI

KLABU ya Simba imesema mchezaji Aboul Karimu kutoka Mali atafanya majaribio na klabu hiyo hivi karibu na kama atafanya vyema hivyo atapewa nafasi ya kuitumikia klabu hiyo ya msimbazi.

Akizungumza na gazeti hili jana jijini Dar es Salaam, Msemaji wa Simba, Ezekiel Kamwaga alisema Simba imekuwa na mazungumzo na wakala wa kimataifa Valer St.Clair kuhusu majaribio ya mchezaji huyo raia wa Mali.

“Endapo atafanikiwa kwenye majaribio anaweza kuwa mchezaji wa mwisho kusajiliwa kwenye dirisha la usajili na hivyo kupata nafasi ya kuitumikia timu ya Simba kwa msimu ujao wa Ligi Kuu Tanzania bara na ligi Mabingwa Afrika,” alisema Kamwaga.
Mchezaji huyo anatarajiwa kutua nchini mwishoni mwa wiki hii na kuanza majaribio wakati dirisha la usajili likiwa linafikia tamati Septemba 10.

Vile vile klabu ya Simba jana ilichukua fursa ya kuwatambulisha wachezaji wake wapya wa kimataifa, MKenya Pascal Ochieng na Mghana Daniel Akuffor.

Kamwaga alisema beki wa kati Pascal Ochieng atachukua majukumu hayo kwenye Ligi Kuu ambayo iko karibuni kuanza wakati Daniel Akuffor atakuwa akiichezea wekundu wa msimbazi kwenye ligi ya mabingwa ya Afrika.

Kamwaga pia alisema Simba imeweka wazi kwamba mkataba wa Mchezaji mpya Daniel Akuffor utamalizika Mei mwakani.

Alisema,“mkataba wetu na Akuffor mwisho mwezi wa tano na hivyo kwenye makubaliano yetu hatacheza Ligi Kuu ila ataiwakilisha Simba kwenye ligi ya mabingwa ya Afrika.”

Simba itashiriki kwenye ligi ya mabingwa Afrika itakayoanza mwaka huu baada ya kutwaa kombe la ligi kuu ya Tanzania bara wakati huo huo timu ya Azam iliyomaliza katika nafasi ya pili itashiriki kwenye kombe la Shirikisho Afrika.

No comments:

Post a Comment