Monday, August 15, 2011

MAN UNITED YAANZA VYEMA LIGI

Bao la kujifunga wenyewe la West Brom dakika za mwisho lilisaidia kumpunguzia mashaka mlinda mlango wa Manchester United David de Gea, wakati Manchester United walipoanza kampeni ya kuutetea ubingwa wake kwa ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya West Brom.
Rooney akishangilia bao
Rooney akishangilia bao

Wayne Rooney alifunga bao la kuongoza mapema kipindi cha kwanza baada ya kugongeana vizuri na Fabio pamoja na Ashley Young na kuachia mkwaju uliomshinda mlinda mlango wa West Brom Ben Foster.
Shane Long akasawazisha katika mechi yake ya kwanza kubwa kwa klabu ya West Brom baada ya mkwaju wake hafifu kupita kwapani mwa mlinda mlango De Gea.
United walipata bao la ushindi baada ya krosi iliyopigwa upande wa kushoto na Ashley Young ikamgonga mlinzi wa West Brom Steven Reid mpira ukajaa wavuni na kumuacha mlinda mlango Ben Foster asijue la kufanya.
Matokeo hayo yameifanya Manchester United kushika nafasi ya pili ikiwa na pointi tatu nyuma ya vinara wa ligi hadi sasa Bolton wenye pointi tatu na mabao manne ya kufunga.

No comments:

Post a Comment