Friday, August 5, 2011

MWANASOKA NAOKI WA JAPAN AFARIKI DUNIA

Mwanasoka mashuhuri wa Japan Naoki Matsuda amefariki dunia siku mbili baada ya kupoteza fahamu uwanjani akiwa mazoezini ikidhaniwa ni matatizo ya moyo.

Marehemu Naoki Matsuda

Matsuda aliyekuwa na umri wa miaka 34, aliyeiwakilisha Japan katika fainali za Kombe la Dunia za mwaka 2002, siku ya Jumanne alikimbizwa.
Alianguka na kuzimia akifanya mazoezi na klabu yake ya Matsumoto Yamaga, na tangu wakati huo hakuweza kurejewa na fahamu.
Meneja wa zamani wa timu ya taifa ya Japan, Philippe Troussier akitoa rambirambi zake kwa familia ya mchezaji huyo, alisema alikuwa mchezaji muhimu katika kikosi cha nchi hiyo kilichoshiriki Kombe la Dunia.
"Inasikitisha sana kuona mtu anafariki dunia akiwa na umri mdogo kama wake," Bw Troussier alieleza Shirika la Reuters.
"Ni pigo kubwa. Alikuwa kijana mzuri sana na nilikuwa karibu naye. Niko pamoja na jamaa zake katika msiba huu mkubwa."
Mashabiki, marafiki na wachezaji wenzake wa zamani, walikusanyika katika hospitali ya Matsumoto kumtakia apone haraka alipokuwa amepoteza fahamu.
Matsuda aliichezea Japan mara 40 na kushinda mataji mara mbili katika Ligi ya nchi hiyo katika kipindi cha miaka 15 cha uchezaji wake na timu ya Yokohama F-Marinos.
Mapema mwaka huu alijiunga na timu ya Matsumoto inayocheza ligi ya chini.

No comments:

Post a Comment