Friday, November 11, 2011

Mwanamama Johnson-Sirlief anaongoza kwa kura je, kuendelea kuiongoza Liberia?

Rais anaetetea kiti chake Liberia Johnson Sirleaf


Wakati kura zinaendelea kuhesabiwa nchini Liberia, rais wa sasa wa nchi hiyo , Ellen Johnson-Sirleaf, anaelekea kupata ushindi wa rahisi katika uchaguzi wa duru ya pili ya rais.

Matokeo ya awali yaliyotolewa na tume ya kitaifa ya uchaguzi imempa Bibi Johnson-Sirleaf ushindi wa zaidi ya asilimia 90 ya kura zote.

Mpinzani wake Winston Tubman amepata asilimia tisa pekee, licha ya wito kwa wafuasi wake kusususia uchaguzi huo.

Bwana Tubman alidai uchaguzi huo ulikumbwa na visa vya udanganyifu katika duru ya kwanza ya upigaji kura, japo waangalizi wa kimataifa wamepinga hilo.


Mpinzani wake Winston Tubman

Bibi Johnson-Sirleaf amesema licha ya idadi ndogo ya watu kujitokeza kupiga kura, matokeo ya uchaguzi huo ni halali.

''Shughuli nzima ya upigaji kura ni halali na hii ni kwa sababu inatosheleza mahitaji ya kikatiba. Tarehe 11 Oktoba watu wa Liberia walipiga kura na japo tulikuwa wagombea 16, asilimia 44 walinipigia kura''. Rais Ellen Johnson-Sirleaf amesema.

Hata hivyo mgombea wa upinzani aliyesusia uchaguzi wa rais wa duru ya pili, Winston Tubman, amepinga uhalali wa uchaguzi huo wa rais, Bwana Tubman amesema ''matokeo yaliyotolewa na tume ya uchaguzi ni ya juu na sidhani walifikisha kiwango hicho''.

Mwandishi wa BBC nchini Liberia anasema kuwa watu wachache walijitokeza kupiga kura.

Takriban thuluthi moja pekee ya wapigaji kura ndio walijitokeza, na hii huenda ikadhoofisha uhalali wa ushindi wa Bibi Johnson-Sirleaf pia, huenda ikazidisha wasiwasi nchini humo.

No comments:

Post a Comment