Wednesday, May 16, 2012

ROBIN VAN PERSIE ANYAKUA KIATU CHA DHAHABU ENGLAND


ROBIN VAN PERSIE NA KIATU CHA DHAHABU

Mshambuliaji wa Arsenal, Robin van Persie(RVP) ametwaa kiatu cha dhahabu msimu huu, kwa kuwashinda Wayne Rooney na Sergio Aguero katika ufungaji.

Mshambuliaji huyo mwenye miaka 28, ametwaa tuzo hiyo kwa mara ya kwanza katika maisha yake, pia amepokea paundi 30,000 kama zawadi yake kwa kushinda tuzo hiyo.


ROBIN VAN PERSIE akishangilia moja ya magoli aliyofunga msimu huu

Van Persie amefunga mabao 30 msimu huu na kufikia rekodi iliyowekwa Arsenal na mkongwe Thierry Henry msimu wa 2003/04, na hiyo ni tuzo yake ya tatu kuipata katika wiki za karibuni baada ya kushinda tuzo ya PFA na Mchezaji bora wa Mwaka inayotolea na Waandishi wa Soka.

Van Persie alikuwa nguzo muhimu kwa 'Gunners' msimu huu, kwa kufunga mabao yaliyoiwezesha timu hiyo kufuzu kwa Ligi ya Mabingwa msimu huu.

Wayne Rooney amemaliza wapili nyuma ya Van Persie akiwa amefunga mabao 27, na watatu ni Aguero mfungaji wa mabao muhimu lililowezesha Manchester City kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu kwa mara ya kwanza baada ya miaka 44.

Mabao mawili ya Van Persie yameingia kwenye kinyang'anyiro cha kuwania tuzo ya bao la msimu, pamoja na lile alilofunga dhidi ya Everton kwenye Uwanja wa Emirates mwezi Desemba.
Wakati huohuo; Klabu ya Arsenal inatarajiwa kumpa mkataba mpya na mnono mshambuliaji wake, Robin van Persie kabla ya kuanza kwa michuano ya Ulaya mwezi ujao.

Mtandao wa Sportpulse umeeleza jana kuwa Van Persie ambaye amemaliza msimu akiwa mfungaji bora kwa mabao 30 atasaini mkataba wa pauni 220,000 kwa wiki wa kuendelea kubaki katika klabu hiyo ya London ambayo mkataba wake unaisha mwakani.

Ofa hiyo, Sportpulse inaeleza kuwa itamfanya kuwa mchezaji anayelipwa kiasi kikubwa Arsenal.

Kulingana na mtandao huo, ofa hiyo itambakisha kwa muda mrefu zaidi katika klabu hiyo pamoja na kuzizuia klabu nyingine kama vile, Real Madrid, Man City na Juventus ambazo zinamtaka.

Van Persie ambaye ameibuka mshindi wa tatu kwa ufungaji mabao Ulaya nyuma ya Lionel Mess (Barcelona) na Cristiano Ronaldo wa Real Madrid amekuwa gumzo msimu huu kwa umahiri wake wa kupachika mabao.

Kocha wa Arsenal, Arsene Wenger amekuwa akieleza kutokuwa tayari kumwachia mshambuliaji huyo raia wa Uholanzi ambaye amekuwa akisumbuliwa na maumivu misimu michache iliyopita.

Msimu huu, mshambuliaji huyo ametwaa tuzo ya mchezaji bora wa Ulaya wa Chama cha Wachezaji wa Kulipa (PFA) na pia Chama cha Waandishi wa Habari za Michezo barani humo.

No comments:

Post a Comment