Friday, June 8, 2012

EURO 2012 NYASI KUANZA KUCHIMBIKA LEO, POLAND Vs UGIRIKI KUFUNGUA PAZIA


Mwenyeji mwenza, Poland leo inaanza kutupa kete zake katika mchezo mgumu wa ufunguzi wa mashindano ya Euro 2012 ikiikaribisha Ugiriki.

Poland imekutana na Ugiriki mara 15 katika mashindano ya Ulaya na mara zote wamekuwa wakiisumbua Ugiriki baada ya kushinda michezo 10, kutoka sare mara mbili na kupoteza mechi tatu walipokutana.

Poland euro 2012 national team
Kikosi cha POLAND

Greece euro 2012 national team
Kikosi cha UGIRIKI

Kikosi cha kocha Franciszek Smuda cha Poland kinaingia dimbani leo kwenye Uwanja wa Taifa mjini Warsaw bila majeruhi tayari kuwakabili mabingwa wa Ulaya mwaka 2004 Ugiriki.

Katika mchezo wa leo, Smuda anatarajiwa kupanga kikosi ambacho kinaongozwa na mshambuliaji Robert Lewandowski anayecheza soka Ujerumani katika kikosi cha Borussia Dortmund ambao ni mabingwa mara mbili wa ligi hiyo.

Lakini, huyu hatakuwa pekee yake ila atasaidiwa na wakali wenzake wa Borussia Dortmund, Lukasz Piszczek na Jakob Blaszczykowski pamoja nao, Rafal Murawski na Eugen Polanski katika kiungo kukiwezesha kikosi hicho maarufu kama 'White Eagles' kuanza kwa malengo.

Lakini, Ugiriki inaingia dimbani kwa matarajio ya kucheza mfumo wa 4-3-3 dhidi ya Poland.

Mchezaji tegemeo atakuwa Vasilis Torosidis ambaye awali alidhaniwa kuwa angezikosa fainali hizo baada ya kuumia katika mchezo wa kirafiki dhidi ya Slovenia wiki iliyopita.

Beki huyo wa kulia amepona na kurejea na yupo tayari kwa mashindano hayo ambayo macho na masikio ya wengi yapo kwa Sotiris Ninis, chipukizi wa miaka 21 ambaye amekuwa akifanya vizuri.

Wengine ni Dimitris Salpingidis ambaye ataongoza mashambulizi ya watu watatu mbele.

Poland au White Eagles walifuzu kwa mara ya kwanza mwaka 2008, lakini walishika mkia katika kundi lao wakiwa na pointi moja.

Pia, kikosi cha Smuda kimecheza mechi tano na kutoruhusu bao na kwa dakika 461 hawajafungwa bao tangu lile la Tamas Priskin katika ushindi wa 2-1 dhidi ya Hungary, Novemba 15, 2011.

Nao Ugiriki ambao hawakuwahi kushinda mechi wakicheza soka Poland walifuzu kushiriki Euro 2012 wakiongoza Kundi F kwa pointi 24 bila kufungwa wakizitangulia Croatia na Israel.

Timu hiyo inao wachezaji watatu pekee kutoka kikosi cha ubingwa cha mwaka 2004 ambao ni, Giorgos Karagounis, Kostas Katsouranis na Kostas Chalkias.

Habari zaidi ya Euro 2012 UK 30.

No comments:

Post a Comment